Picha na Rahel Pallangyo.



STRAIKA wa Simba, Amisi Tambwe leo amefunga bao lake la kumi katika Ligi Kuu ya Bara, lakini mkongwe Saidi Maulid ‘SMG’ amedhihirisha kwamba bado ni moto wa kuotea mbali huku kipa Amani Simba akilimwa ‘red card’ iliyowaacha wengi midomo wazi.
Simba ilikuwa ikicheza kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam dhidi ya Ashanti na kuibuka na ushindi wa mabao 4-2 lakini mchezaji wake Tambwe raia wa Burundi amefikisha idadi ya mabao 10 na kuongoza katika orodha ya wafungaji wa ligi hiyo.
Kabla ya mchezo huo, Tambwe alikuwa ameshafunga mabao tisa akifuatiwa na Hamisi Kiiza wa Yanga mwenye mabao manane. Wengine wanaofuatia ni Elius Maguri wa Ruvu Shooting, Juma Liuzio wa Mtibwa Sugar na Kipre Tchetche wa Azam wenye mabao saba kila mmoja.
Tambwe alifunga bao lake dakika ya 46 akiunganisha pasi safi ya Ramadhan Singano ‘Messi’ ambaye aliwanyanyasa mabeki wa Ashanti upande wa kushoto kisha kutoa pasi safi kwa mfungaji aliyefunga kirahisi.
Akizungumza na mtandao huu mara baada ya mchezo huo, Tambwe alisema anashukuru kufunga mabao 10 hadi sasa na anawashukuru wachezaji wenzake ndani ya Simba na benchi la ufundi kwa ushirikiano waliompa hadi akafiksiha idadi hiyo ya mabao.
“Kazi yangu siku zote ni kufunga, nadhani kama mchezaji natumia vyema nafasi ninazopata kuweza kufunga na kufanya mambo kuwa mazuri kwa watu wote. Nafanya haya (kufunga) kwa faida ya Simba na watu wote wanaoipenda klabu hii,” anasema Tambwe.



 Picha na Rahel Pallangyo.


SMG HATARI…
Winga Said Maulid ‘SMG’ wa Ashanti United leo amedhihirisha kwamba bado yupo katika kiwango chake baada ya kucheza vyema nafasi hiyo dhidi ya Simba na kufanya vizuri.
SMG aliweza kucheza vyema mbele ya beki Issa Rashid maarufu kama Baba Ubaya na kuonyesha bado yumo kiasi ambacho alikuwa akishangiliwa mara kwa mara na mashabiki waliokuwepo uwanjani hapo.
“Nadhani nalinda kiwango changu kwa kufanya mazoezi mara kwa mara tofauti na wachezaji wengine ambao wakiona umri umeenda anajibweteka na kuachana na soka,mimi sipo hivyo ndiyo maana leo umeniona nacheza vile,” anasema SMG aliyewahi kuzichezea Simba na Yanga kwa nyakati tofauti miaka ya mwanzoni ya 2000.
Katika mchezo huo, SMG aliifungia Ashanti bao la pili dakika ya 52 akiunganisha vyema krosi kutoka wingi ya kulia na kuamsha shamra shamra miongoni mwa mashabiki wa Ashanti licha ya timu yao kuwa nyuma kwa mabao 3-2 kabla ya Betram Mombeki hajaifungia Simba bao la nne.
AMANI SIMBA APIGWA RED CARD…
Kipa wa zamani wa Simba, Amani Simba ambaye leo aliichezea Ashanti United, alionyeshwa kadi nyekundu dakika ya 89 baada ya kuudaka mpira akiwa nje ya eneo lake analoruhusiwa.
Mwamuzi Andrew Shamba wa Pwani alimwonyesha Amani kadi hiyo baada ya kuudaka mpira uliopigwa na Ramadhan Singano ‘Messi’ wa Simba baada ya Simba kucheza shambulizi la ghafla huku mabeki wa Ashanti wakiwa wamepandisha timu.
Messi aliiwahi pasi ya kutoka kwa mabeki wa timu yake na kumiliki mpira kisha akawa anamfuata Amani langoni kwake, lakini kwa kutambua hatari inayomfuata kipa huyo akaliacha lango lake na kumfuata Messi ambaye aliunyanyua mpira lakini ghafla Amani akanyoosha mikono yake na kujikuta ameudaka.
Baada ya kuudaka mpira huo, Amani aliduwaa kwa sekunde kama mbili hivi kisha akauachia na moja kwa moja akaanza kuvua grovu zake huku akijua lazima ataonyeshwa kadi nyekundu kutokana kitendo chake hicho.
Mara baada ya mchezo huo, Amani aliuambia mtandao huu kwamba, hakudhamili kuudaka mpira ule lakini pia hakujua kama Messi angepiga juu kidogo na yeye kumfikia mikononi.
“Mimi nilijua atapiga chini halafu nilale ili nimzuie sasa wakati najipanga kufanya hivyo yeye akapiga na mpira ukaja mikononi mwangu, sikuwa na jinsi n ndipo nikaudaka na moja kwa moja nikavua glovu kwani nilijua lazima nionyeshwe kadi nyekundu,” anasema Amani.  

SIMBA YAIFANYIA MAUAJI ASHANTI, MOMBEKI APIGA MBILI TAIFA


    Picha kwa hisani ya Rahel Pallangyo.

LICHA ya kubaki katika nafasi ya nne kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya Bara, mashabiki wa klabu ya soka ya Simba leo jioni walitoka kifua mbele kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam baada ya timu yao kuibuka na ushindi wa mabao 4-2 dhidi ya Ashanti United. 

Matokeo hayo yanaifanya Simba kubaki katika nafasi ya nne ikiwa na pointi 24 baada ya kucheza mechi 13, huku iksihinda mechi sita, kutoka sare sita na kufungwa moja. Ashanti yenyewe imebaki na pointi zake 10 baada ya kucheza mechi 13 pia. 

Ashanti iliyoanza ligi kwa kusuasua, imeshinda mbili, imetoka sare nne na kufungwa mechi saba. Imefunga mabao 12 na kufungwa 24. 

Simba iliingia uwanjani na kumbukumbu ya sare ya bao 1-1 dhidi ya Kagera Sugar, lakini iliwachukua dakika nane tu kupata bao la kwanza lililofungwa na Ramadhan Singano maarufu kama Messi akimalizia mpira wa pasi ndefu kutoka katikati ya uwanja. 

Baada ya kuingia kwa bao hilo, Ashanti walikuja juu na kutaka kusawazisha lakini ukuta wa Simba ulioongozwa na Gilbert Kaze ulikuwa makini kuondosha hatari zote zilizoelekezwa kwao. 

Wakati mashabiki wakidhani timu hizo zitaenda kupumzika huku Simba ikiongoza kwa bao moja, dakika ya 45 Ashanti ilipata bao la kusawazisha lililofungwa na Hussein Sued aliyemalizia krosi safi ya Joseph Malunda. 

Hadi mwamuzi Andrew Shamba kutoka Pwani anapuliza filimbi ya mapumziko, timu hizo zilikuwa sawa kwa bao 1-1. 

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi lakini walikuwa Simba waliotumia vyema mabadiliko yaliyofanywa na kocha Abdallah Kibadeni baada ya kuwatoa Henry Joseph na Amri Kiemba na nafasi zao kuchukuliwa na Said Ndemla na William Lucian kwani dakika ya 46, Amis Tambwe aliipatia Simba bao la pili akimalizia kazi nzuri ya Messi. 

Dakika tatu baadaye, mshambuliaji Betram Mombeki aliipatia Simba bao la tatu akimalizia pasi safi ya beki Haruna Shamte, hata hivyo dakika ya 52 Said Maulidi ‘SMG’ aliipatia Ashanti bao la pili akimalizia krosi safi kutoka wingi ya kulia. 

Simba ilipata bao la nne dakika ya 60 mfungaji akiwa Mombeki baada ya mabeki wa Ashanti kushindwa kumzuia Messi aliyewalamba chenga na kuwazidi nguvu mara kadhaa mabeki wa timu hiyo. 

Katika hali ya kushangaza kila Simba ilipokuwa ikipata bao wachezaji wake walikuwa wakishangilia kwa mtindo wa kuomba msamaha kwa mashabiki wa timu hiyo ambao leo walikuwa chini ya ulinzi mkali wa polisi baada ya mchezo uliopita dhidi ya Kagera kuvunja baadhi ya viti vya uwanja huo.


Matokeo mengine ya ligi kuu ya Vodacom

JKT RUVU 1:0 COASTAL UNION

RUVU SHOOTING 2:2 MTIBWA SUGAR

KAGERA SUGAR 2:0 MGAMBO SHOOTING
Categories:

0 comments:

Post a Comment

    Blogger news

    Blogroll

    Pages

    About